Mark 10

Mafundisho Kuhusu Talaka

(Mathayo 19:1-12; Luka 16:18)

1 aIsa akaondoka huko, akavuka Mto Yordani, akaenda sehemu za Uyahudi. Umati mkubwa wa watu ukaenda kwake tena, naye kama ilivyokuwa desturi yake, akawafundisha.

2 bBaadhi ya Mafarisayo wakaja ili kumjaribu kwa kumuuliza, “Je, ni halali mtu kumwacha mke wake?”

3Isa akawajibu, “Je, Musa aliwaamuru nini?”

4 cWakajibu, “Musa aliruhusu kwamba mume anaweza kumwandikia mkewe hati ya talaka na kumwacha.”

5 dIsa akawaambia, “Musa aliwaandikia sheria hiyo kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu. 6 eLakini tangu mwanzo wa uumbaji, ‘Mungu aliwaumba mwanaume na mwanamke. 7 fKwa sababu hii mwanaume atamwacha baba yake na mama yake na kuambatana na mkewe, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.’ 8 gKwa hiyo hawatakuwa wawili tena, bali mwili mmoja. 9Basi, alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe.”

10Walipokuwa tena ndani ya nyumba, wanafunzi wake wakamuuliza kuhusu jambo hili. 11 hAkawajibu, “Mtu yeyote amwachaye mkewe na kuoa mke mwingine, anazini naye. 12 iNaye mwanamke amwachaye mumewe na kuolewa na mume mwingine, anazini.”

Isa Anawabariki Watoto Wadogo

(Mathayo 19:13-15; Luka 18:15-17)

13 jWatu walikuwa wakimletea Isa watoto wadogo ili awaguse, lakini wanafunzi wake wakawakemea. 14 kIsa alipoona yaliyokuwa yakitukia, akachukizwa. Akawaambia wanafunzi wake, “Waacheni watoto wadogo waje kwangu, wala msiwazuie, kwa maana Ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hawa. 15 lAmin, nawaambia, mtu yeyote asiyeupokea Ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo, hatauingia kamwe.” 16 mAkawachukua watoto mikononi mwake, akawakumbatia, akaweka mikono yake juu yao, akawabariki.

Kijana Tajiri

(Mathayo 19:16-30; Luka 18:18-30)

17 nIsa alipokuwa anaondoka, mtu mmoja akamkimbilia, akapiga magoti mbele yake, akamuuliza, “Mwalimu mwema, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?”

18Isa akamwambia, “Mbona unaniita mwema? Hakuna yeyote aliye mwema ila Mungu peke yake. 19 oUnazijua amri: ‘Usiue, usizini, usiibe, usishuhudie uongo, usidanganye, waheshimu baba yako na mama yako.’ ”

20Akamjibu, “Mwalimu, amri hizi zote nimezishika tangu nikiwa mtoto.”

21 pIsa akamtazama na kumpenda, akamwambia, “Umepungukiwa na kitu kimoja. Nenda ukauze kila kitu ulicho nacho uwape maskini hizo fedha, nawe utakuwa na hazina mbinguni. Kisha njoo, unifuate.”

22Yule mtu aliposikia hayo, akasikitika sana. Akaondoka kwa huzuni kwa sababu alikuwa na mali nyingi.

23 qIsa akatazama pande zote, akawaambia wanafunzi wake, “Itakuwa vigumu sana kwa wenye mali kuingia katika Ufalme wa Mungu!”

24 rWanafunzi wake wakashangazwa sana na maneno hayo. Lakini Isa akawaambia tena, “Wanangu, tazama jinsi ilivyo vigumu kwa wale wanaotumainia mali kuingia katika Ufalme wa Mungu. 25 sNi rahisi zaidi kwa ngamia kupita kwenye tundu la sindano kuliko mtu tajiri
Tajiri ina maana wale wanaotumainia mali.
kuingia katika Ufalme wa Mungu.”

26Wanafunzi wake wakashangaa sana. Wakaulizana wao kwa wao, “Ni nani basi awezaye kuokoka?”

27 uIsa akawatazama, akawaambia, “Kwa mwanadamu jambo hili haliwezekani, lakini kwa Mungu sivyo. Mambo yote yanawezekana kwa Mungu.”

28 vNdipo Petro akamjibu, “Tazama, tumeacha kila kitu na kukufuata wewe!”

29Isa akasema, “Amin, nawaambia, hakuna mtu yeyote aliyeacha nyumba, ndugu wa kiume au wa kike, au mama au baba, au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili, 30 wambaye hatalipwa mara mia katika ulimwengu huu: nyumba, ndugu wa kiume na wa kike, mama na baba na watoto, mashamba pamoja na mateso, kisha uzima wa milele katika ulimwengu ujao. 31 xLakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho, na wa mwisho watakuwa wa kwanza.”

Isa Atabiri Mara Ya Tatu Kufa Na Kufufuka Kwake

(Mathayo 20:17-19; Luka 18:31-34)

32 yWalikuwa njiani wakipanda kwenda Yerusalemu, na Isa alikuwa ametangulia. Wanafunzi wake walishangaa, nao watu waliowafuata walijawa na hofu. Isa akawachukua tena wale wanafunzi wake kumi na wawili kando na kuwaambia yatakayompata. 33 zAkasema, “Tunapanda kwenda Yerusalemu, na Mwana wa Adamu atasalitiwa kwa viongozi wa makuhani na walimu wa sheria. Wao watamhukumu kifo na kumtia mikononi mwa watu wa Mataifa, 34 aaambao watamdhihaki na kumtemea mate, watampiga na kumuua. Siku tatu baadaye atafufuka.”

Ombi La Yakobo Na Yohana

(Mathayo 20:20-28)

35 abKisha Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo, wakaja kwake na kumwambia, “Mwalimu, tunataka utufanyie lolote tutakalokuomba.”

36Naye akawaambia, “Je, mwataka niwafanyie jambo gani?”

37 acWakamwambia, “Tupe kukaa mmoja upande wako wa kuume na mwingine upande wako wa kushoto katika utukufu wako.”

38 adLakini Isa akawaambia, “Ninyi hamjui mnaloliomba. Je, mnaweza kukinywea kikombe ninyweacho mimi, au kubatizwa ubatizo nibatizwao mimi?”

39 aeWakajibu, “Tunaweza.”

Kisha Isa akawaambia, “Kikombe nikinyweacho mtakinywea na ubatizo nibatizwao mtabatizwa,
40lakini kuketi mkono wangu wa kuume au wa kushoto si juu yangu mimi kuwapa. Nafasi hizi ni kwa ajili ya wale walioandaliwa.”

41 afWale wanafunzi wengine kumi waliposikia hayo, wakaanza kuwakasirikia Yakobo na Yohana. 42 agLakini Isa akawaita wote pamoja na kuwaambia, “Mnafahamu kuwa wale wanaodhaniwa kuwa watawala wa watu wa Mataifa huwatawala watu kwa nguvu, nao wenye vyeo huonyesha mamlaka yao. 43 ahLakini isiwe hivyo kwenu. Badala yake, yeyote anayetaka kuwa mkuu miongoni mwenu hana budi kuwa mtumishi wenu, 44na yeyote anayetaka kuwa wa kwanza, hana budi kuwa mtumwa wa wote. 45 aiKwa kuwa hata Mwana wa Adamu hakuja ili kutumikiwa, bali kutumika na kuutoa uhai wake uwe fidia kwa ajili ya wengi.”

Isa Amponya Kipofu Bartimayo

(Mathayo 20:29-34; Luka 18:35-43)

46 ajKisha wakafika Yeriko. Isa alipokuwa akiondoka mjini na wanafunzi wake pamoja na umati mkubwa wa watu, kipofu mmoja, jina lake Bartimayo, mwana wa Timayo, alikuwa ameketi kando ya njia akiomba msaada. 47 akAliposikia kuwa ni Isa Al-Nasiri aliyekuwa anapita, akaanza kupaza sauti akisema, “Isa, Mwana wa Daudi, nihurumie!”

48Watu wengi wakamkemea, wakamwambia akae kimya, lakini yeye akazidi kupaza sauti, akisema, “Mwana wa Daudi, nihurumie!”

49Isa akasimama na kusema, “Mwiteni.”

Hivyo wakamwita yule mtu kipofu, wakamwambia, “Jipe moyo! Inuka, anakuita.”
50Akiwa analivua lile joho lake, alisimama na kumwendea Isa.

51 alIsa akamuuliza, “Unataka nikufanyie nini?”

Yule kipofu akajibu, “Mwalimu, nataka kuona.”

52 amIsa akamwambia, “Nenda zako, imani yako imekuponya.” Mara akapata kuona, akamfuata Isa njiani.
Copyright information for SwhKC